Twitter inaanzisha mfumo mpya wa kubaini na kuondoa machapisho yanayopotosha kuhusu chanjo ya COVID-19 na kuwafungia watumiaji watakaoonekana kusisitiza kuenea kwa habari za uongo.
Kampuni hiyo imesema inaamini hatua hiyo itasaidia kupunguza madhara yatakayotokana na kuenezwa kwa taarifa potofu kupitia jukwaa lake.
Mfumo huo utahusisha kuwajulisha watumiaji ikiwa chapisho litakuwa na taarifa potofu kuhusu maambukizi ya Corona Virus hasa chanjo, ikiweka alama kuwa taarifa iliyopo katika chapisho hilo si sahihi.
Mwaka jana, Twitter ilitoa wito kwa watumiaji kuondoa machapisho yanayotoa taarifa zisizo sahihi, na tangu hapo imeondoa machapisho 8,400 na kuwajulisha watumiaji zaidi ya Milioni 11.5 duniani kuhusu kukiuka taratibu.