Ushirikiano wa kukabili janga la Corona kati ya serikali ya Kaunti ya Turkana na ile ya Kitaifa huenda ukadidimia baada ya madereva wa magari ya masafa marefu kuruhusiwa kuingia kaunti hiyo bila kufanyiwa vipimo vya Corona.
Akizungumza kwenye maadhimisho ya miaka 57 ya sherehe za madaraka katika eneo la Ekales mjini Lodwar Naibu gavana kaunti ya Turkana Peter Lotethiro amesema afisi ya kaunti kamishna kaunti hiyo imeonekana kulegeza kamba dhidi ya masharti ambayo yamewekwa na kamati ya kaunti iliyobuniwa kukabili maambukizi zaidi ya ugojwa wa COVID-19.
Ni matamshi ambayo yamepuuliwa mbali na kaunti kamishna kaunti ya Turkana Muthama Wambua akitaja hatua ya kuweka agizo la kuzuia kutoka wala kuingia kaunti ya Turkana kuwa kinyume cha sheria na hakuna kiongozi yeyote katika ngazi ya kaunti mwenye mamlaka ya kuweka agizo hilo.
Kulingana na Muthama ni jukumu la viongozi katika kaunti ya Turkana kufuata njia mwafaka za kisheria ili kuhakikisha agizo la kutoingia au kutoka kaunti hiyo linatekelezwa kikamilifu na serikali kuu.
Hata hivyo ni jambo ambalo limepelekea wakaazi wa kaunti ya Turkana kutishia kufunga barabara ya Lodwar-Kitale katika eneo la Kainuk ili kuzuia magari ya masafa marefu kuingia kaunti hiyo hadi pale serikali itakapoanza zoezi la kuwapima madereva hao kabla ya kuruhusiwa kuingia kaunti hiyo.