Msanii wa Gengetone Sylvia Ssaru ambaye pia anatajwa kama mmoja wa marapa wenye vipaji nchini anadaiwa kuwa kwenye ugomvi na meneja wake wa zamani baada ya kutokuwa na maelewano mazuri.
Inasemekana, meneja wa Ssaru anayefahamika kwa jina la Kennedy Oluchi amemtaka msanii huyo amlipe shilingi Milioni 1.5 ili ampe idhini ya kutumia channel yake ya Youtube ambayo ina zaidi ya wafuasi 78,000.
Kwa sasa, chaneli hiyo ya YouTube imeondolewa, na haipo hewani wakati huu tunachapisha taarifa hii.
Chanzo cha karibu na wawili hao kimezungumza na ukurasa wa udaku wa Nairobi club na kutoa maelezo yote kuhusu bifu kati ya rapa huyo na meneja wake wa zamani ambaye anadaiwa anataka alipwe “haki yake” kabla ya kumrudishia Ssaru chaneli yake ya YouTube.
Hata hivyo Sylvia Ssaru bado hajatoa taarifa rasmi kuhusu ishu ya kutokuwa na maelewano mazuri na meneja wake huyo ambaye amekuwa akisimamia kazi zake kwa muda mrefu.
Purukushani kati ya wawili hao inakuja siku chache baada ya mama wa msanii Trio Mio, Irma Sakwa kukata uhusiano na meneja wa mtoto wake, Wilkings Fadhili baada ya kudaiwa kuwa alimtapeli mwanawe zaidi ya shilling 100,000.