Katika maeneo kame, kuendeleza kilimo biashara huwa ni changamoto kubwa lakini kwenye eneo la na Napuu ,kaunti ndogo ya Turkana ya Kati kuna mradi wa kilimo ambao unaendelezwa katika eneo kame la Natoot na umeonyesha ustawi mkubwa.
Mradi huo ambao ulianzishwa na Shirika la Brightop International kwa ushirikiano na Kanisa la Full Gospel kaunti ya Turkana mwaka wa 2017 umewafaidi zaidi ya wakulima 70 kwenye kaunti ndogo ya turkana ya kati.
Kulingana na mshirikishi wa shirika la Brightop International Victor Juma mradi huo unatekelezwa kwenye shamba la ekari 4 ambalo lilitolewa na jamii ya eneo hilo baada ya kupata ari ya kuendeleza kilimo umwagiliaji maji mashamba.
Aidha amesema licha ya changamoto wamefaulu kuwahamasisha wakulima kuhusu umuhimu wa mradi huo wa Natoot na umeleta matumaini mengi kwa wakazi sehemu hiyo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Muungano wa Makanisa ya Full Gospel eneo la Nawoitorong Kaunti ya Turkana, Simon Loote amesema kuwa bado wanapitia changamoto kadhaa ambazo ni ukosefu wa vifaa vya kisasa vya unyunyizaji mashamba maji pamoja na uhaba wa maafisa wa nyanjani ambao wanafaa kuwapatia ushauri kuhusu kilimo bora.
Hata hivyo wakulima waliofaidia na mradi huo umwagiliaji maji mashamba wamesema kilimo hicho kimebadilisha maisha yao kwani kwa sasa wameanza kuuza mazao yao ili kuwasaidia kujikumu kimaisha.