Mgombea wa chama cha Forum for Democratic Change (FDC) Erias Lukwago ametangazwa mshindi kwenye uchaguzi wa Umeya wa jiji la Kampala, akimbwaga mwanamuziki Joseph Mayanja maarufu kama Jose Chameleone.
Lukwago amefanikiwa kutetea kiti chake, baada ya kupata kura 194,592. Mwanasiasa huyo ambaye pia ni wakili amekuwa Meya wa jiji la Kampala tangu Januari 14, mwaka 2011.
Mgombea wa chama cha National Unit Platform (NUP) Nabillah Naggayi Sempala ameshika nafasi ya pili kwa kupata kura 60,082. Daniel Kazibwe maarufu “Ragga Dee” wa chama cha NRM amekuwa wa tatu kwa kupata kura 23,388 wakati Jose Chameleone ambaye alikuwa kwenye kinyang’anyiro cha kiti cha Umeya Jiji la Kampala kama mgombea huru amepata kura 12,212.