Vijiji sita vilivyoko kaunti ya ndogo ya Turkana ya Kati vinatarajiwa kunufaika na mradi wa maji unaoendeshwa na Shirika lisiokuwa la Practical Action katika kipindi cha miezi mitatu ijayo.
Akizungumza wakati wa kusambaza maji katika eneo la Lokaparaparai viungani mwa mji wa Lodwar, Afisa katika Shirika la Practical Action Joel Ombok amesema wamechukua hatua hiyo baada ya kubaini kuwa vijiji hivyo vinakumbwa na uhaba mkubwa wa maji hasa kipindi hiki cha corona.
Aidha amesema mradi huo ambao wameshirikiana na Idara ya maji kaunti ya Turkana unalenga kusambaza maji mara mbili kwa mwezi ili kuwasaidia wakaazi maeneo hayo kuzingatia usafi kipindi hiki cha mapambano dhidi ya janga la corona.
Hata hivyo wakaazi wa Lokaparaparai wadi ya Lodwar township wamepongeza hatua ya Shirika la Practical Action kupitia serikali ya kaunti ya Turkana kuwaletea maji katika eneo hilo huku wakitoa wito kwa uongozi wa kaunti kuweka mikakati zaidi kukabili tatizo la maji ambalo limekumba eneo hilo kwa muda mrefu sasa.