Serikali ya Kaunti ya Turkana imebuni kamati ya kupambana na tishio la ugonjwa wa Corona katika kaunti hiyo.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari Naibu Gavana kaunti ya Turkana Peter Lotethiro amesema jukumu la jopo hilo ni kuhakikisha wananchi wanahamasishwa kuhusu ugonjwa huo wa corona.
Kwa upande wake Waziri wa Afya kaunti hiyo Jane Ajele amesema tayari wamepokea vifaa vya kupambana na Corona huku akisema maafisa wa afya kaunti hiyo wamepokezwa mafunzo yatakayowasaidia kukabiliana na virusi vya COVID-19.
Hata hivyo kamishna wa kaunti ya Turkana Muthama Wambiua amepiga marufuku mikutano yote ya hadhara kufuatia tishio la ugonjwa wa Corona huku akiwaonya wananchi dhidi ya kujikusanya katika makundi.