Idara ya usalama katika Kaunti ya Turkana imeahidi kuimarisha usalama katika kambi ya wakimbizi ya Kakuma baada ya kisa cha kwanza cha corona kuripotiwa eneo hilo..
Kamanda mkuu wa polisi kaunti ya turkana Samuel Ndanyi amesema kuwa tayari maafisa wa polisi zaidi wametumwa kushika doria eneo hilo ili kuhakikisha kuwa hakuna anayeingia na kutoka katika kambi hiyo kipindi hiki cha tishio la corona.
Aidha ndanyi amesema maafisa wake wako macho katika kila pembe ya kaunti hiyo ikizingatiwa kuwa malori sita ya masafa marefu kutoka Sudan Kusini yanashikiliwa katika eneo la Nadapal kutokana na hatua ya madereva wa malori hayo kufeli kutoa na vyeti vinavyoonyesha kuwa hawana maambukizi ya virusi vya covid-19.
Hata hivyo amesema iwapo madereva wa malori hayo watasita kuwasilisha stakabadhi hitaji kwa muda unaofaa, watalazimika kuwarejesha walikotoka hadi pale watakapowasilisha vyeti vya kudhibitisha kwamba hawana maambukizi ya corona ndipo wataruhusiwa kuingia nchini.